Home Blog

Mganga wa tiba asili akamatwa kwa tuhuma za mauaji Kibaha

0

Na Mwandishi Wetu, Pwani

Jeshi la Polisi mkoa wa Pwani linamshikilia Ally Shabani (29), mganga wa tiba asili na mkazi wa Makazi Mapya, Mlandizi wilayani Kibaha, kwa tuhuma za mauaji ya Juma Nyambihira.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani, Muhudhwari Msuya, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), alisema tukio hilo lilifichuka baada ya ndugu wa marehemu kutoa taarifa ya kupotea kwake tangu Agosti 17. Taarifa hizo zilikabidhiwa Kituo cha Polisi Mlandizi mnamo Agosti 29, mwaka huu.

Kwa mujibu wa ACP Msuya, baada ya taarifa hizo polisi walifungua jalada la uchunguzi na kuanza kufuatilia. Hatua hiyo ilimfikisha mikononi mwao mtuhumiwa Shabani, ambaye inadaiwa alikuwa akiishi na marehemu Juma akimpatia matibabu ya asili kutokana na tatizo la uoni hafifu.

Mwili Wapatikana Katika Shimo

Kamanda Msuya alieleza kuwa mnamo Septemba 3, wakati upelelezi ukiendelea, askari walifika nyumbani alipokuwa akiishi mtuhumiwa pamoja na marehemu kwa ajili ya upekuzi. Katika eneo hilo, walibaini uwepo wa tanuri la mkaa lililokuwa karibu na nyumba hiyo, ambapo kando yake kulionekana dalili za shimo.

“Baada ya kufukuliwa, tulibaini ndani ya shimo hilo ulikuwa mwili wa marehemu Juma Nyambihira,” alisema ACP Msuya.

Mwili wa marehemu unatarajiwa kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu kabla ya kukabidhiwa kwa ndugu kwa taratibu za mazishi.

Mtuhumiwa Kufikishwa Mahakamani

Jeshi la Polisi limeeleza kuwa mtuhumiwa Ally Shabani atafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi kukamilika, huku likiendelea na hatua za uchunguzi ili kubaini undani wa tukio hilo.

Mkurugenzi Bangu: Ajira 31,875 zimezalishwa kupitia WRS

0

Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRS) umezalisha ajira 31,875 katika mwaka wa fedha 2025/26 kupitia shughuli mbalimbali za mnyororo wa thamani wa mazao na bidhaa.

Hayo yameelezwa leo jijini Dodoma na Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) Asangye Bangu katika mkutano na waandishi wa habari ulioandaliwa na Idara ya Habari – MAELEZO wa kutangaza utekelezaji wa shughuli za kwa mwaka wa fedha 2025/26 na mwelekeo wa mwaka 2026/27.

Bangu, amesema ajira hizo zimetokana na shughuli za ukusanyaji wa mazao na bidhaa, uhifadhi ghalani, upimaji wa ubora, usafirishaji, upakiaji na upakuaji pamoja na huduma nyingine zinazohusiana na biashara kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Aidha, amesema mchango wa WRRB katika kuongeza mapato ya Serikali umeendelea kuimarika, ambapo fedha zilizorejeshwa katika Mfuko Mkuu wa Serikali zimeongezeka kutoka Sh. milioni 22 mwaka wa fedha 2023/24 hadi kufikia Sh. milioni 140 mwaka 2025/26.

Akizungumzia kuhusu ukaguzi wa bidhaa, Bangu amesema katika mwaka wa fedha 2025/26, magunia 19,041,651 yenye uzito wa zaidi ya kilo bilioni 1.114 yalikaguliwa katika ghala mbalimbali nchini, hatua iliyochangia kuimarisha uaminifu wa mfumo na kulinda maslahi ya wadau wote wa biashara.

WRRB yaja na mikakati mitano ya kukuza mfumo wa stakabadhi za ghala

0

Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imetangaza maeneo matano ya kimkakati itakayoyatekeleza katika kipindi cha miaka mitano ijayo kuanzia mwaka wa fedha 2026/27 hadi 2030/31, yenye lengo la kuimarisha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, kupanua huduma zake na kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Asangye Bangu, ameyasema hayo leo jijini Dodoma katika mkutano na waandishi wa habari ulioandaliwa na Idara ya Habari – MAELEZO.

Amesema maeneo hayo ya kimkakati ni kupanua mfumo katika sekta mpya za uzalishaji, kuongeza matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA), kuimarisha ushiriki wa taasisi za fedha, kuongeza uwekezaji katika miundombinu ya maghala na huduma za biashara, pamoja na kuendelea kutoa elimu, kuutangaza na kuukuza Mfumo wa Stakabadhi za Ghala. 

Bangu amesema katika mkakati wa kupanua mfumo, WRRB itaanza kuingiza sekta ya mifugo katika Mfumo huo kuanzia mwaka wa fedha 2026/27, ambapo mnada wa kwanza wa mifugo kupitia mfumo huo unatarajiwa kufanyika Wilaya ya Mvomero.

Aidha, amesema bidhaa nyingine zikiwemo mwani, ngozi, mazao ya bustani na bidhaa nyingine zitakazokidhi vigezo zitaendelea kujumuishwa katika mfumo huo. 

Amesema WRRB pia itaendelea kuboresha mifumo ya kidijitali ikiwemo WRS-MIS, WRMS na matumizi ya stakabadhi za kielektroniki ili kuongeza uwazi, ufanisi na kurahisisha utoaji wa huduma kwa wadau wa mfumo. 

Kadhalika, amesema Bodi itaendelea kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania, benki za biashara na taasisi nyingine za fedha ili kuongeza upatikanaji wa mikopo inayotumia stakabadhi za ghala kama dhamana. 

Pamoja na hayo, Mkurugenzi Bangu amewahamasisha wawekezaji kuwekeza katika ujenzi na uendeshaji wa maghala ya kisasa ili kuongeza uwezo wa nchi kuhifadhi bidhaa kwa usalama, kupunguza upotevu na kuongeza ushindani katika masoko ya ndani na kimataifa. 

Ameongeza kuwa utekelezaji wa mikakati hiyo utaongeza matumizi ya mifumo ya kidijitali katika biashara, kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi, kuongeza ajira, mapato ya Serikali na Halmashauri, pamoja na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupitia biashara yenye ushindani, uwazi na tija.

Hali ngumu kiuchumi yawasukuma vijana kutumiwa kisiasa

0

Imeelezwa kuwa hali ngumu ya kiuchumi imewasababisha vijana wengi kukumbwa na msongo wa mawazo na kujikuta wakitumiwa vibaya na baadhi ya wanasiasa.

Kauli hiyo imetolewa na Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Mhashamu Wolfgang Pisa, kando ya Mkutano wa 21 wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati (AMECEA), unaofanyika jijini Nairobi, Kenya.

Mhashamu Pisa amesema hali hiyo pia inawasukuma vijana wengi kukumbwa na shinikizo la kuhama nchini kutafuta fursa katika maeneo mengine, jambo alilosema ni hatari ikiwa hawatatayarishwa vizuri.

Pisa, ambaye pia ni Askofu wa Jimbo Katoliki Lindi, amesisitiza umuhimu wa kuzungumza na vijana mara kwa mara kupitia njia mbalimbali, ikiwamo mitandao ya kijamii, na kuwahamasisha kutumia mitandao hiyo kwa njia sahihi.

“Wengine ni wahanga wa mazingira kwa sababu ya uchumi, na moja ya matatizo makubwa ni mambo mawili. Kutokana na hizo changamoto, moja ni wanasiasa, wanasiasa wanaotumia vijana kufikisha malengo yao, lakini vijana kwa sababu hawana uchaguzi mkubwa katika uchumi, wakati mwingine ni aidha nijiunge au nitakufa njaa,” ameeleza Pisa.

Amesema kuna haja ya kuwaweka vijana hao karibu na kuwapa ushauri na maelekezo ili wasitumbukie katika tatizo hilo.

TRA yawanoa waajiriwa wapya kuzingatia weledi katika utendaji kazi

0

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imewataka waajiriwa wake wapya kuzingatia weledi, nidhamu na maadili ya utumishi wa umma ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa walipakodi.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Elimu kwa Mlipakodi na Mawasiliano wa TRA, Richard Kayombo, wakati akifungua mafunzo elekezi kwa waajiriwa wapya yanayofanyika katika Chuo cha Kodi, jijini Dar es Salaam.

Kayombo alisema mtumishi wa TRA anapaswa kutekeleza majukumu yake kwa uadilifu, kuwaheshimu walipakodi na watumishi wenzake, huku akisisitiza kuwa nidhamu ndiyo msingi wa mafanikio katika utendaji wa kazi.



Maadili, weledi, kuzingatia kanuni na taratibu za utumishi wao ni nguzo muhimu katika utendaji kazi ndani ya TRA na kutoa huduma bora kwa walipakodi na wananchi kwa ujumla, alisema.

Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea waajiriwa wapya uelewa wa majukumu yao, maadili ya utumishi na utamaduni wa kazi ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania ili waanze majukumu yao kwa ufanisi.

BAVICHA yahoji matumizi ya mashtaka ya ugaidi

0

Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la CHADEMA (BAVICHA), Deogratias Mahinyila, ametoa wito kwa Watanzania na wadau mbalimbali kushirikiana kuhakikisha hali ya matumizi ya tuhuma za ugaidi dhidi ya wananchi inakomeshwa, akidai kuwa imekuwa ikitumiwa kuwabambikia watu kesi na kulichafua taifa.

Akizungumza leo katika ofisi za zamani za CHADEMA zilizopo Ufipa, Dar es Salaam, Mahinyila amesema kuwa utaratibu wa kuwasingizia na kuwabambikia wananchi kesi za ugaidi hauna haki na unaweza kuharibu taswira ya Tanzania ndani na nje ya nchi.

Amedai kuwa kauli zinazotolewa kuhusu uwepo wa ugaidi nchini zinazua hofu miongoni mwa wananchi na zinaweza kudhoofisha uhusiano wa Tanzania na mataifa mengine pamoja na kuathiri mazingira ya uwekezaji na utalii.

Mahinyila alisema taarifa zilizowahi kutolewa na Jeshi la Polisi zinaonyesha kuwa zaidi ya watu 130 wanakabiliwa na tuhuma za ugaidi, akisisitiza kuwa hali hiyo si jambo la kawaida kwa taifa na inapaswa kutazamwa kwa umakini.

Amehoji mantiki ya kauli zinazodai kuwa Tanzania haina ugaidi wakati kuna watu wanaoshikiliwa na kushtakiwa kwa makosa hayo, akidai kuwa baadhi ya watuhumiwa hao wanakabiliwa na mashtaka yasiyo ya kweli.

Aidha, ameeleza kuwa matumizi ya kesi za ugaidi yanaweza kuwa na athari kwa taswira ya Tanzania kimataifa, akidai pia kuwa yanaweza kuathiri maandalizi ya michuano ya AFCON kutokana na umuhimu unaowekwa na vyombo vya michezo duniani katika masuala ya haki za binadamu.

Samia begins official visit to Angola to deepen bilateral ties

0

President Samia Suluhu Hassan departed Tanzania on Friday for a two-day official working visit to Angola at the invitation of President João Lourenço, in a trip aimed at strengthening the longstanding relationship between the two countries.

During the visit, President Samia and President Lourenço will jointly inaugurate the Julius Kambarage Nyerere Referral Hospital in Luanda. The ceremony is expected to be attended by members of the late Mwalimu Julius Nyerere’s family, led by Mama Maria Nyerere, in recognition of his pivotal role in Africa’s liberation struggles.

Samia is also scheduled to hold bilateral talks with President Lourenço to discuss ways of expanding cooperation in key sectors and advancing issues of mutual interest between Tanzania and Angola.

As part of her programme, President Samia will attend a fundraising gala dinner organised by the spouses of African heads of state. The initiative seeks to raise funds for social and economic programmes that support the empowerment of women and young people across Africa.

According to a statement from the Presidency, the visit underscores the shared commitment of Tanzania and Angola to further strengthen their historic partnership, built during the struggle for the liberation of southern Africa and sustained through decades of close diplomatic cooperation.

Rais Samia akutana na Mama Maria Nyerere safarini Angola uzinduzi  Hospitali ya Nyerere

0

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Mama Maria Nyerere muda mfupi kabla ya kuanza safari ya kuelekea Luanda, Angola ambapo anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya Uzinduzi wa Hospitali iliyopewa jina la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tarehe 31 Julai, 2026.

Mkuranga yapanua Shule kukabiliana na ongezeko la wanafunzi 

0

Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani imeanza mkakati wa kujenga shule za msingi na sekondari za ghorofa kwa kutumia mapato ya ndani, hatua inayolenga kuongeza nafasi za wanafunzi na kukabiliana na ongezeko la mahitaji ya elimu.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Waziri Kombo, amesema katika mwaka wa fedha 2026/2027, Sh bilioni 1.7 zimetengwa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Shule ya Sekondari Mwandege, huku ujenzi wa Shule ya Sekondari Muungano ukiwa pia sehemu ya mpango huo.

Amesema Sh bilioni 2.1 zinatumika katika ujenzi wa Shule ya Msingi Mwandege ya ghorofa yenye vyumba 16 vya madarasa, huku mchakato wa ujenzi wa shule hiyo ukiendelea na mkandarasi akiwa tayari amepatikana kwa ajili ya shule ya sekondari.

Kombo amesema miradi hiyo itagharamiwa kupitia vyanzo vya mapato vya ndani, ikiwemo eneo la maegesho ya malori lenye ukubwa wa ekari 50 pamoja na mapato yatakayopatikana kupitia upangishaji wa eneo la bandari kavu.

Amesema Halmashauri itaendelea kusimamia na kuimarisha vyanzo hivyo ili kupata fedha za kugharamia ujenzi wa miundombinu ya elimu.

Kwa mujibu wa Kombo, ujenzi wa madarasa ya Shule ya Msingi Mwandege unatarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa mwaka huu. Shule hiyo kwa sasa ina vyumba 12 vya madarasa, hivyo kukamilika kwa jengo jipya kutaongeza nafasi kwa idadi kubwa ya wanafunzi.

Amesema ongezeko la wanafunzi linatarajiwa kuwa kubwa kutokana na mabadiliko ya sera ya elimu, hivyo Halmashauri imejipanga kuongeza madarasa na kujenga shule mpya, hususan katika kata za Mwandege, Vikindu, Vianzi na Mipeko ambazo zina idadi kubwa ya wanafunzi.

Kombo amewataka wazazi na wadau wa elimu kushirikiana na Serikali kwa kuchangia mahitaji madogo ya shule, akisema Serikali inaendelea kugharamia elimu bila ada pamoja na mahitaji makuu ya uendeshaji.

Amesema lengo ni kuhakikisha wanafunzi wote watakaofaulu wanapata nafasi ya kuendelea na Kidato cha Kwanza, huku ujenzi wa shule za ghorofa ukitarajiwa kuongeza uwezo wa Halmashauri kuhudumia ongezeko hilo la wanafunzi.

Minada ya ufuta yawaongezea wakulima mapato

0

Ubora wa ufuta unaozalishwa mkoani Pwani umeendelea kuchangia kuongezeka kwa bei katika minada, ambapo kilo moja imefikia Sh2,720 katika mnada wa sita uliofanyika katika Ghala Kuu la Kibiti.

Meneja wa CORECU Mkoa wa Pwani, Hamis Mantawela, amesema bei hiyo imeongezeka ikilinganishwa na mnada wa tano, ambapo kilo moja iliuzwa kwa bei ya juu ya Sh2,500.

Amesema katika mnada wa sita zaidi ya tani 400 za ufuta ziliuzwa, huku bei ya chini ikiwa Sh2,370 kwa kilo. Aidha, hadi kufikia mnada wa tano, zaidi ya Sh bilioni 30 zilikuwa zimelipwa kwa wakulima.

Mantawela amewataka wakulima na wadau ambao bado wana ufuta majumbani kuufikisha katika maghala ili uweze kushiriki katika minada rasmi, akisema hatua hiyo inaweza kuongeza ushindani na kuchochea bei kupanda zaidi.

Amesema minada hiyo inaendeshwa kwa uwazi kwa kuwa wakulima wanapata fursa ya kufuatilia mchakato wa mauzo, huku akibainisha kuwa hadi kufikia mnada wa tano hakukuwa na mkulima aliyekuwa akidai malipo.

Kwa upande wa bei kwa wilaya, Mkuranga iliongoza kwa Sh2,720 kwa kilo, ikifuatiwa na Kibiti Sh2,673.12, Bagamoyo, Chalinze na Kisarawe Sh2,616, huku Rufiji ikiuzwa kwa Sh2,554.32.

Afisa Rasilimali Watu wa TMX, Haikael Mkongo, amesema mfumo wa kidijitali umeongeza uwazi katika mauzo kwa kumwezesha mnunuzi na mkulima kufuatilia bei ya zao hilo kupitia simu.

Amewataka wakulima ambao bado hawajapeleka ufuta kwenye maghala kufanya hivyo ili wanufaike na mfumo wa minada ya kidijitali, ambao pia huokoa muda kwa wakulima na wanunuzi.

Ajali ya Makuyuni yaua sita, wengine wajeruhiwa

0

Watu sita wamefariki dunia na wengine kadhaa kujeruhiwa katika ajali mbaya iliyohusisha basi la Kampuni ya Kandahari na malori mawili katika eneo la Makuyuni, Wilaya ya Monduli mkoani Arusha.

Ajali hiyo ilitokea usiku wa Julai 30, 2026, wakati basi la Kandahari lenye namba za usajili T 732 DRL, lililokuwa likitoka Kilimanjaro kuelekea Mpanda mkoani Katavi, lilipogongana uso kwa uso na semi-trela yenye namba T 727 EPW, iliyokuwa ikitoka Kahama kuelekea Tanga.

Kwa mujibu wa mashuhuda, dereva wa basi alijaribu kulipita lori lililokuwa mbele yake katika eneo lenye kona, lakini kutokana na mwonekano hafifu wa barabara alikutana uso kwa uso na semi-trela iliyokuwa ikitokea upande wa pili.

Nguvu ya mgongano huo ilisababisha basi hilo kuharibika vibaya, huku baadhi ya abiria wakinaswa ndani ya gari. Dereva wa basi na abiria wengine walifariki katika ajali hiyo, huku majeruhi wakikimbizwa hospitalini kwa matibabu.

Lori jingine lenye namba T 757 DWV, lililokuwa likifuata semi-trela hiyo, lilipinduka wakati dereva wake alipokuwa akijaribu kukwepa ajali.

Vikosi vya uokoaji vikishirikiana na Jeshi la Polisi, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na wasamaria wema vilifika eneo la tukio na kufanya operesheni ya kuwaokoa majeruhi, kutoa miili ya waliopoteza maisha na kuondoa magari yaliyoharibika.

Ajali hiyo ilisababisha msongamano mkubwa wa magari katika Barabara Kuu ya Arusha–Babati kwa saa kadhaa wakati shughuli za uokoaji na usafishaji wa barabara zikiendelea.

Hadi taarifa hii inaandaliwa, Jeshi la Polisi lilikuwa halijatoa taarifa rasmi kuhusu idadi kamili ya majeruhi, huku uchunguzi ukiendelea kubaini chanzo cha ajali na kuthibitisha takwimu za waathirika.