Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linamshikilia Baraka Hassani Juma (19), mkazi wa Kagongwa, Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga, kwa tuhuma za kumtorosha mwanafunzi wa kidato cha pili mwenye umri wa miaka 14, ambaye jina lake limehifadhiwa kwa mujibu wa sheria.
Kwa mujibu wa taarifa ya Polisi, tukio hilo lilitokea Januari 5, 2026, katika Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam, ambapo mtuhumiwa alidaiwa kummdanganya na kumtorosha binti huyo kinyume cha sheria.
Baada ya ufuatiliaji, Polisi walimkamata mtuhumiwa Januari 17, 2026, katika nyumba ya kulala wageni eneo la Ukonga Mombasa, akiwa pamoja na mwanafunzi huyo, wakijiandaa kusafiri kuelekea Kagongwa, Kahama mkoani Shinyanga.
Jeshi la Polisi limesema hatua za kisheria zinaendelea kuchukuliwa dhidi ya mtuhumiwa kwa kushirikiana na mamlaka husika ili haki itendeke kwa mujibu wa sheria.
Akizungumza kuhusu tukio hilo, SACP Faustine Mafwele amesema Polisi haitasita kuwachukulia hatua kali za kisheria wote watakaobainika kujihusisha na vitendo vya uhalifu, hususan unyanyasaji na ukatili dhidi ya watoto.




