Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara imetangaza kuwafungia michezo mitano wachezaji wa Simba SC, Jonathan Sowah na Allasane Kanté, pamoja na kuwatoza faini ya Shilingi milioni moja kila mmoja.
Kwa mujibu wa uamuzi huo, Sowah amepata adhabu hiyo kutokana na kumpiga kiwiko kiungo wa Azam FC, Himid Mao, wakati Kanté akihukumiwa kwa kosa la kumpiga teke la makusudi kiungo wa Azam FC, Feisal Salum.
Katika uamuzi mwingine, Kamati hiyo pia imemfungia michezo mitano kiungo wa Singida Black Stars, Khalid Aucho, kwa kosa la kumpiga na kumsukuma Adam Adam wa TRA United. Aucho pia atalipa faini ya Shilingi milioni moja.
Aidha, Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi imetozwa adhabu nyingine kwa Klabu ya Yanga, ambayo imepewa faini ya Shilingi milioni tano kutokana na kosa la shabiki wake kuingia uwanjani na kufanya vitendo visivyoruhusiwa wakati wa mchezo.
Kamati hiyo imewakumbusha wachezaji, klabu na mashabiki kuzingatia kanuni, sheria na maadili ya mchezo ili kulinda taswira ya Ligi Kuu Tanzania Bara.




