Thursday, March 12, 2026
spot_img
HomeBiasharaBolt, LATRA wajadili udhibiti sheria usafiri mtandao

Bolt, LATRA wajadili udhibiti sheria usafiri mtandao


Bolt Tanzania imekutana na Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) kwa kushirikiana na wawakilishi wa Kikosi cha Usalama Barabarani katika kikao cha ngazi ya juu kilicholenga kujadili masuala ya udhibiti na uzingatiaji wa sheria katika sekta ya usafiri wa mtandao nchini.

Kikao hicho pia kililenga kubaini suluhu za vitendo zitakazochochea ukuaji endelevu wa sekta hiyo pamoja na kuongeza ushirikishwaji wa wadau mbalimbali.

Katika kikao hicho, Bolt iliwasilisha mkakati wake wa soko kwa mwaka 2026, unaolenga kuongeza idadi ya madereva na abiria kwa takriban asilimia 40, kuanza rasmi huduma zake Zanzibar na kupanua huduma katika miji mingine ya Tanzania Bara.

Kampuni hiyo ilieleza kuwa kwa sasa inatoa huduma katika miji minane nchini, ikiwemo Mwanza, Morogoro, Mbeya na Tanga.

Katika kuimarisha ukuaji wa mfumo wa usafiri wa mtandao, Bolt imeonesha utayari wa kushirikiana na wadhibiti kurahisisha upatikanaji wa leseni za kibiashara kwa madereva. Hatua hiyo itahusisha pia kampeni ya pamoja ya “Drive to Compliance” inayolenga kuongeza uelewa wa sheria, kurahisisha mchakato wa urasimishaji na kukuza ushiriki salama katika sekta hiyo.

Akizungumza katika kikao hicho, Meneja Mkuu wa Bolt Afrika Mashariki, Dimmy Kanyankole, alisema lengo la kampuni hiyo ni kushirikiana kwa karibu na wadhibiti ili kukuza mfumo mzima wa sekta ya usafiri wa mtandao.

“Ukuaji endelevu lazima uambatane na uzingatiaji wa sheria, haki na urasimishaji ulio thabiti,” alisema Kanyankole.

Kwa upande wake, Mkuu wa Udhibiti na Sera wa Bolt Afrika, Weyinmi Aghadiuno, alisema kikao hicho ni sehemu ya dhamira ya kampuni katika kukuza uwazi na majadiliano yanayozingatia ushahidi.

Alisema ushirikiano wa karibu kati ya wadhibiti na sekta binafsi utaimarisha uadilifu wa udhibiti, kuhakikisha bei za haki na kurahisisha uendeshaji wa madereva katika maeneo yote wanayofanya kazi.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa LATRA, Halima Lutavi, alisema mamlaka hiyo iko tayari kuendeleza majadiliano yenye tija yatakayolinda usalama, uzingatiaji wa sheria na haki katika sekta hiyo huku ikiunga mkono ubunifu wa kiteknolojia.

Majadiliano hayo pia yaligusia ujumuishaji wa mifumo ya kiteknolojia (API integration), uthibitishaji wa leseni kwa wakati halisi, upatikanaji wa maeneo ya biashara katikati ya miji kwa waendesha bodaboda, utekelezaji wa tozo za kisheria pamoja na mikakati ya kudhibiti safari zinazofanyika nje ya mfumo wa programu ili kuimarisha usalama na kulinda mapato ya serikali.

Pande zote mbili zilikubaliana kuendelea na vikao vya kila robo mwaka pamoja na kampeni za uhamasishaji kwa madereva, kwa lengo la kuhakikisha uwazi wa kanuni na ustawi wa muda mrefu wa sekta ya usafiri wa mtandao inayokua kwa kasi nchini. 🚖

RELATED ARTICLES

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

- Advertisment -
NMB Tanzania

Most Popular

Recent Comments