Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Dk. James Mwainyekule, amewataka watumishi wa Ofisi hiyo kutekeleza majukumu yao kwa weledi na uadilifu wa hali ya juu ili kukidhi matarajio ya Watanzania kwa ufanisi na tija zaidi.
Ametoa rai hiyo leo 17 Desemba 2025 wakati wa kikao cha baraza la Wafanyakazi wa EWURA kilichofanyika mkoani Singida.
“ Tufanye kazi kwa ushirikiano, tutoe huduma kwa weledi na tuendelee kuwa waadilifu. Tukumbuke pia sisi ni timu moja, tuepuke majungu na manung’uniko mahali pa kazi kwani husababisha kutokuelewana na hivyo kuathiri utendaji,” alisema Dkt. Mwainyekule.




Aliongeza kuwa wafanyakazi wote wana wajibu wa kutekeleza majukumu yao kwa uwazi, ufanisi na tija ili kuhakikisha ubora na upatikanaji endelevu wa huduma za umeme, mafuta, gesi asilia na maji na usafi wa mazingira.
“Ifahamike kuwa, baraza la wafanyakazi ni chemchemi ya mawazo mapya. Tutafanya mabadiliko ya namna tunavyofanya kazi, ili tuendane na wakati wa sasa, hatuwezi kufanya kazi kama ambavyo tulifanya miaka iliyopita,” alisema.
Naibu Katibu Mkuu TUGHE Taifa, Mha. Amani Msuya, aliipongeza EWURA kwa maandalizi mazuri ya kikao cha baraza la wafanyakazi na kwa kulipa umuhimu suala la ushirikishwaji wafanyakazi.








