Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, leo amewasili katika Ukumbi wa Kiramuu, Mbezi Juu, mkoani Dar es Salaam, kuendelea na ziara yake ya kukutana na kuzungumza na Mabalozi wa Mashina kwa lengo la kuimarisha uhai, mshikamano na utendaji wa Chama ngazi ya mashina.
Ziara hiyo inafanyika chini ya kauli mbiu “Shina Lako Linakuita”, ikiwa na dhamira ya kukifikia chama kuanzia ngazi ya chini kabisa, ambapo uhai wa CCM unaanzia. Kupitia ziara hiyo, Balozi Dkt. Migiro anatarajiwa kutembelea Wilaya zote za Mkoa wa Dar es Salaam na kusikiliza changamoto, maoni na mapendekezo ya wanachama.




Awali, Katibu Mkuu huyo alianza ziara yake katika Wilaya za Temeke na Kigamboni, huku leo akiendelea na mikutano katika Wilaya za Kinondoni na Ubungo. Ziara hiyo inatarajiwa kuhitimishwa rasmi Januari 13, 2026, katika Wilaya ya Ilala.








