📌…Rais Samia awatandika milioni 40, Kabudi awapongeza mashabiki
Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Hemed Morocco amesema ushindi wa 2-0 dhidi ya Burkina Faso ni mwanzo tu, akiahidi makubwa zaidi kutoka kwa kikosi chake kwenye fainali za CHAN 2025.

Akizungumza baada ya mechi ya ufunguzi iliyopigwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, Morocco alisema Stars ina kikosi bora kuliko wakati mwingine wowote na anaamini watakwenda mbali kwenye michuano hiyo.
“Tumeanza vizuri, tunahitaji kuimarika kila mechi. Tunajua tulikuwa na changamoto ya ufungaji, lakini tumejipanga,” alisema Morocco.
Stars inatarajiwa kurudi uwanjani Jumatano dhidi ya Mauritania katika Kundi B linalojumuisha pia Afrika ya Kati na Madagascar.
Wakati huo huo, Rais Samia Suluhu Hassan ametoa shilingi milioni 40 kwa Stars kama motisha baada ya ushindi huo.
Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Paramagamba Kabudi, aliwakabidhi wachezaji fedha hizo, na kuongeza kiasi cha milioni 20 kutoka Wizara yake.
Kabudi aliipongeza timu na mashabiki kwa kujitokeza kwa wingi na kusema ni wakati wa kupigania ubingwa.
Mashindano hayo yanafanyika kwa ushirikiano wa Tanzania, Kenya na Uganda.