Mbunge wa zamani wa Jimbo la Kisesa, Mkoa wa Simiyu, Luhaga Mpina, sasa ni mwanachama halali wa Chama cha ACT-Wazalendo na tayari amekabidhiwa fomu ya kuwania nafasi ya Urais wa chama hicho.

Kwa mujibu wa taarifa za uhakika kutoka ndani ya ACT-Wazalendo, Mpina alikabidhiwa rasmi kadi ya uanachama pamoja na fomu ya kugombea urais siku ya Jumatatu, Agosti 4, 2025.
Hatua hiyo inafungua ukurasa mpya wa kisiasa kwa Mpina, ambaye jina lake lilikatwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika mchakato wa ndani wa uteuzi wa wagombea ubunge kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, mwaka huu.
Wakati taarifa za kujiunga kwake na ACT-Wazalendo zikisambaa, chama hicho leo, Agosti 5, kimeendesha vikao muhimu vya Kamati ya Uongozi, Kamati Kuu na Halmashauri Kuu Taifa, vikijadili maandalizi ya Mkutano Mkuu wa chama utakaofanyika kesho, Jumatano, Agosti 6.
Picha zilizosambaa mitandaoni zimemwonesha Mpina akisajiliwa kidijitali na Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Dorothy Semu. Katika picha hizo pia alikuwepo Kiongozi wa zamani wa chama hicho, Zitto Kabwe, ambapo wote walionekana wakitabasamu kwa furaha.















