Klabu ya Yanga imesema hakuna mchezaji aliyehakikishiwa namba ya kudumu kwenye kikosi, na nafasi itatokana na juhudi na ufanisi wa mchezaji kuingia kwenye mfumo wa kocha Romain Folz.

Ofisa Habari wa Yanga, Ali Kamwe, alisema hayo kufuatia usajili wa beki wa kushoto Mohamed Hussein ‘Tshabalala’, ambaye amerejea Ligi Kuu akitokea Simba SC. Kamwe alisema nafasi ya kucheza itatolewa kulingana na mazoezi na mahitaji ya kocha, si jina au timu aliyotoka mchezaji.
Tshabalala anakwenda kuungana na wachezaji wengine wa upande wa kushoto kama Shadrack Boka, Nickson Kibabage na Israel Mwenda.
Aidha, Kamwe alithibitisha kuwa kikosi cha Yanga kimeanza rasmi kambi ndani ya Tanzania kwa maandalizi ya msimu ujao, na kinatarajiwa kucheza mechi ya kirafiki dhidi ya Rayon Sports ya Rwanda Agosti 15, katika Uwanja wa Amahoro, Kigali.




