Thursday, March 5, 2026
spot_img
HomeHabariFamilia ya watu watatu yateketea kwa moto Musoma

Familia ya watu watatu yateketea kwa moto Musoma


Watu watatu wa familia moja wamefariki dunia akiwemo mtumishi wa Wizara ya Maji, Rochi Mkolekuwa (39), baada ya nyumba yao kuteketea kwa moto katika Mtaa wa Nyarusrya, Manispaa ya Musoma, Mkoa wa Mara.

Mbali na Mkolekuwa, aliyekuwa Meneja wa Ubora wa Maji katika Maabara ya Mkoa wa Mara, wengine waliofariki dunia katika tukio hilo ni mkewe Mariam Msigwa (34) pamoja na mtoto wao Rochi Shaban (4).

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mara, Agostino Magere, amesema chanzo cha moto huo bado hakijajulikana na kwamba uchunguzi wa kina umeanza mara moja.

Magere amesema Jeshi la Zimamoto lilipokea taarifa za tukio hilo saa 10 usiku wa kuamkia leo, Jumatatu Januari 5, 2026, na walipofika eneo la tukio walikuta nyumba hiyo ambayo familia hiyo ilikuwa ikiishi tayari imeteketea kwa moto, huku watu wote watatu wakiwa bado ndani.

“Inaonekana taarifa ilichelewa kutolewa. Tulipofika eneo la tukio tulikuta tayari wote wamefariki dunia. Mwili wa baba ulikutwa sebuleni, huku miili ya mama na mtoto ikikutwa chumbani. Uchunguzi unaendelea kwa kushirikiana na vyombo vingine vya usalama,” amesema Magere.

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limewataka wananchi kutoa taarifa mapema pindi wanapobaini matukio ya moto ili kuepusha hasara ya maisha na mali.

RELATED ARTICLES

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

- Advertisment -
NMB Tanzania

Most Popular

Recent Comments