Desemba Mosi kila mwaka ni maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani, ambapo katika kuadhimisha siku hiyo, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umetoa msaada wa mahitaji mbalimbali ikiwemo vyakula kwa watoto wenye uhitaji wanaolelewa kwenye Kituo cha Kijiji cha Matumaini jijini Dodoma.
Maafisa kutoka Mfuko huo wakiongozwa na Afisa Tawala Mkuu wa PSSSF, Rose Irresa walikabidhi msaada huo wenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 6 uliojumuisha vyakula, nguo na mahitaji mengine muhimu.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Irresa alisema, siku zote PSSSF imekuwa ikiunga mkono juhudi za kusaidia makundi mbalimbali ya kijamii kama watoto hawa wenye uhitaji.


“Mkurugenzi Mkuu ametuelekeza tuitumie siku hii ya Maadhimisho ya Ukimwi, tufike hapa ili kushirikiana na wanajumuiya wa hapa kwa kuwafariji watoto wetu.” amesema Irresa.
Kwa upande wake mlezi wa Kituo hicho Sista Christina Shilagi ameishukuru PSSSF kwa msaada huo na kwamba wameupokea kwa furaha kubwa.
Amesema mpaka sasa kituo hicho kinalea watoto 163 na kati ya hao wapo wamaosoma shule za msingi, sekondari na vyuo vikuu.
“Kituo hiki kimefanikiwa kuendelea kulea watoto hawa wenye uhitaji kwa kushirikiana na wasamaria wema ambao wamekuwa wakitoa miasada ya vitu mbalimbali kama hivi ambavyo tumepokea leo.” amesema Sista Shilagi.






