Wachezaji wa Yanga wameahidiwa bonasi kubwa endapo watafanikiwa kuibuka na ushindi kwenye mchezo wa raundi ya tano ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya AS FAR ya Morocco, utakaochezwa kesho jijini Rabat.
Ofisa Habari wa klabu hiyo, Ali Kamwe, amesema ahadi hiyo imetolewa na mdhamini wa klabu, Ghalib Said Mohamed (GSM), kwa lengo la kuongeza morali na ushindani kwa wachezaji katika mchezo huo wa maamuzi.
Kamwe amesema wachezaji wamehamasika na kuahidi kupambana kwa nguvu zote ili kupata ushindi, huku kiasi cha bonasi kikiwa hakijawekwa wazi. Ameongeza kuwa maandalizi yanaendelea vizuri licha ya uchovu wa safari ndefu, huku wachezaji wakifanya mazoezi mepesi ya kuondoa uchovu.
Mchezo huo ni wa muhimu kwa timu zote ambazo zina pointi tano kila moja, ambapo mshindi ataweka mguu mmoja kwenye hatua ya robo fainali. Sare inaweza kuinufaisha zaidi Yanga kutokana na ushindi wa bao 1-0 walioupata kwenye mchezo wa kwanza Dar es Salaam. Aidha, mechi hiyo itachezwa bila mashabiki baada ya AS FAR kufungiwa na CAF.




