Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umefanya vikao kazi na Maafisa Usimamizi wa Rasilimali Watu na Utawala pamoja na Maafisa Fedha (Wahasibu) katika mikoa ya Ruvuma na Kagera, Novemba 19, 2025, kwa lengo la kueleza maboresho yaliyotekelezwa na kusisitiza matumizi ya huduma za mtandaoni kupitia mfumo wa PSSSF Kidijitali.
Katika maelezo yao baada ya vikao hivyo, washiriki wamesema hatua ya Mfuko kuwafikia watumishi waliopo pembezoni mwa nchi ni muhimu, na wameahidi kushirikiana kikamilifu kuhakikisha wanachama wanapata huduma bora kwa wakati na kwa mujibu wa sheria.
Akizungumza kwa niaba ya washiriki, Grace Mafuru alisema kuwa kama kiungo kati ya mtumishi na Mfuko, wameelezwa umuhimu wa kuwasilisha taarifa sahihi za mwanachama kwenye mfumo kuanzia anapoanza ajira. Hatua hiyo itasaidia kuondoa usumbufu usio wa lazima na kuharakisha upatikanaji wa huduma.


PSSSF imeweka msisitizo kwamba zaidi ya asilimia 95 ya huduma zake zinapatikana mtandaoni, hivyo Maafisa hao wametakiwa kuwahamasisha watumishi kutumia huduma za kidijitali ili kuokoa muda na gharama. Kupitia huduma hizi, mwanachama anaweza kujihudumia mwenyewe kupata taarifa za michango, mafao, kuwasilisha madai au kuuliza maswali akiwa popote na wakati wowote.
Kwa upande wake, Meneja wa PSSSF Kanda ya Kusini, Sayi Lulyalya, alisema Maafisa Rasilimali Watu na Utawala ndiyo daraja kati ya watumishi na Mfuko, kwani wanahusika moja kwa moja na taarifa za mwanachama tangu anapoajiriwa hadi kustaafu. Kwa sababu hiyo, Mfuko umeweka mkakati maalum wa kuwafikia, kuwapa elimu na kuwahudumia ili kurahisisha utekelezaji wa majukumu yao kwa manufaa ya wanachama.




Naye Meneja wa PSSSF Kanda ya Ziwa Magharibi, Thomas Labi, akiwaeleza washiriki Bukoba, alisema Mfuko umehuisha mafao kwa wastaafu wote kwa asilimia 2, huku wastaafu wanaopokea kima cha chini cha shilingi 150,000 sasa wakifikia 250,000 kuanzia Julai 2025.
Aliongeza kuwa Mfuko pia unatoa shilingi 500,000 kama msaada wa mazishi mara mstaafu anapofariki, na wategemezi wake watalipwa mkupuo wa pensheni ya miezi 36.





