● Lengo ni kusafirisha tani milioni 2.4 kwa mwaka
● Lengo ni kupunguza muda wa usafarisha madini kutoka siku14 hadi siku 5
Kitwe – Zambia
Serikali ya Tanzania na Zambia zimeazimia kuongeza kasi ya uboreshaji wa miundombinu ya usafirishaji wa madini ili kuchochea ukuaji wa sekta ya madini katika ukanda wa Kusini mwa Afrika.
Hatua hiyo ilisisitizwa Machi 25, 2026 na Naibu Waziri wa Madini Dk. Steven Kiruswa wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 13 wa Kimataifa wa Madini na Nishati nchini Zambia (ZIMEC 2026) unaofanyika katika mji wa Kitwe.
Dk. Kiruswa alisema kuwa, mradi wa uboreshaji wa reli ya TAZARA itakuwa suluhisho la kudumu la kupunguza gharama za usafirishaji wa madini ya shaba na kobati kutoka Zambia kwenda soko la dunia kupitia Bandari ya Dar es Salaam nchini Tanzania.




Kiruswa alieleza kuwa, kupitia maboresho ya reli ya TAZARA kutawezesha usafirishaji wa madini ya shaba na kobati kwa wakati ikiwa pamoja na kufika sokoni kwa haraka na gharama nafuu.
Awali, wakati akifungua mkutano Waziri wa Migodi na Maendeleo ya Madini nchini Zambia , Paul Kabuswe aliwataka wawekezaji kutumia fursa ya maboresho ya sera yanayofanywa na nchi hizi mbili ili kuwekeza katika viwanda vya uongezaji thamani ya madini (smelters and refineries) ndani ya ukanda wa nchini za kusini badala ya kusafirisha madini ghafi.
Mkutano wa ZIMEC unatarajiwa kuhitimishwa leo Machi 26, 2026 kwa kutoa azimio la pamoja litakalosisitiza ushirikiano wa kikanda katika kulinda mazingira na kuhakikisha wananchi wa nchi hizo mbili wanafaidika na rasilimali zao.





