Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amefanya mabadiliko makubwa katika Baraza lake la Mawaziri kwa kuongeza idadi ya wizara kutoka 18 hadi 20, hatua inayolenga kuimarisha ufanisi na tija katika utekelezaji wa majukumu ya serikali.
Akitangaza mabadiliko hayo leo Ikulu ya Zanzibar, Dk. Mwinyi alisema marekebisho hayo ni ya kimuundo, yakihusisha kugawa baadhi ya wizara na kuunda wizara mpya ili kuongeza uwiano wa kazi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.




Aidha, katika baraza hilo jipya, mawaziri wawili waliokuwa wakihudumu katika serikali iliyopita — Tabia Maulid Mwita na Ali Suleiman Mrembo — hawajarejeshwa kwenye nafasi zao.
Baraza jipya la mawaziri linatarajiwa kuapishwa Jumamosi, Novemba 15, 2025, katika Ikulu ya Zanzibar, mara tu taratibu zote za kikatiba zitakapokamilika.
Dk. Mwinyi alisisitiza kuwa serikali yake itaendelea kuweka msisitizo katika uwajibikaji, uwazi na utendaji unaolenga matokeo, akiwataka mawaziri wapya kufanya kazi kwa bidii na kushirikiana kwa karibu na wananchi ili kuharakisha maendeleo ya Zanzibar.









