Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), Bernadetta Ndunguru, amesema utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo 2014 toleo la mwaka 2023 unaendelea kuzaa matunda, jambo linalodhihirishwa na umahiri na ubunifu unaooneshwa na wanafunzi wa elimu ya amali katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (Sabasaba).
Akizungumza leo Julai 12, 2026, katika banda la NACTVET, baada ya kutembelea mabanda ya baadhi ya taasisi zinazosimamiwa na Baraza, Ndunguru alisema, elimu ya amali imeanza kubadili mtazamo wa vijana kutoka kutafuta ajira kwenda kuwa wabunifu, wajasiriamali na waajiri.




Alitolea mfano wa umahiri na ubunifu uliooneshwa na mwanafunzi wa amali kutoka Shule ya Sekondari ya Wavulana Bwiru mkoani Mwanza, katika fani ya ujenzi kwa kuonesha mfano wa nyumba ya gharama nafuu na makadirio ya gharama za ujenzi.
Akiwa katika mabanda ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT), Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi( VETA), Ndunguru alijionea bunifu mbalimbali zinazolenga kutatua changamoto za jamii na kukuza uchumi. Miongoni mwa bunifu hizo ni utengenezaji wa vipuri vya bajaji kwa kutumia chupa za plastiki zilizotumika.
Amesema mafanikio haya yanaonesha mchango wa elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi katika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuzalisha wahitimu wenye ujuzi, ubunifu na uwezo wa kujiajiri na kuajiri wengine.






