Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza linawashikilia wahamiaji haramu 14 raia wa Burundi walioingia nchini kinyume cha sheria kupitia magari mawili ya abiria, katika operesheni zilizofanyika wilayani Sengerema.
Akitoa taarifa hiyo leo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, DCP Wilbrod Mutafungwa, alisema mafanikio hayo yametokana na ufuatiliaji wa mienendo ya kihalifu na uwekaji wa vizuizi barabarani ambavyo vimeongeza udhibiti wa uhamiaji haramu.
Ameeleza kuwa katika Kijiji cha Busisi, Tarafa ya Sengerema, wahamiaji haramu 13 walikamatwa Novemba 23, 2025 majira ya saa 7:30 mchana wakiwa ndani ya gari aina ya Tata lenye namba za usajili T 337 DYA, mali ya Chiza Francis Lugubi, mkazi wa Dodoma, ambalo husafiri kati ya Kabanga (Ngara, Kagera) na Mwanza.
Wakati wa kukamatwa, dereva wa gari hilo, Jonas Richard, alitoroka na juhudi za kumtafuta zinaendelea.

Polisi pia wamewakamata watuhumiwa wawili wanaodaiwa kuhusika katika usafirishaji wa wahamiaji hao:
- Mustahper Emily (24), fundi magari mkazi wa Kahama, Shinyanga
- Pendo Matembere (36), kondakta mkazi wa Nyegezi, Mwanza
Baada ya mahojiano, ilibainika kuwa wahamiaji hao waliingia nchini kupitia mpaka wa Kabanga mkoani Kagera mnamo Novemba 22, 2025.
Mtuhumiwa wa 14, Shadia Japhari Majaliwa (18), raia wa Burundi na mkazi wa Kisuru, alikamatwa katika eneo la Nyatukala wilayani Sengerema akiwa ndani ya gari aina ya Yutong lenye usajili T 131 DRE.
Magari yote mawili yanashikiliwa na Jeshi la Polisi huku uchunguzi zaidi ukiendelea ili kubaini mtandao mzima wa usafirishaji haramu wa watu.


Orodha ya wahamiaji waliokamatwa
- Nkurunzinza Eloi (38) – Mhuhutu, Muyinga
- Bizimana Aster (20) – Mhuhutu, Muyebe
- Tanishaga Renova (20) – Mhuhutu, Muyebe
- Nyosaba Anatory (23) – Mhuhutu, Muyebe
- Niyokuru Jlock (23) – Mhuhutu, Muyebe
- Nsolimana Evariste (30) – Mhuhutu, Ngozi
- Riyazimana Jerome (30) – Mhuhutu, Ngozi
- Mbonipa Claude (23) – Mhuhutu, Ngozi
- Ntirampera Oleste (42) – Mhuhutu, Nyanzalaki
- Mbalishimana Swalidi (47) – Mhuhutu, Kitega
- Sindobizero Osca (28) – Mhuhutu, Tangala
- Irakize Derise (27) – Mhuhutu, Ngozi
- Elias Sinilemeya (31) – Mhuhutu, Kitega
- Shadia Jafhari (18) – Mrundi, Kisuru
Kamanda Mutafungwa amesema Jeshi la Polisi litaendelea kuimarisha doria na vizuizi barabarani kwa kushirikiana na vyombo vingine vya usalama pamoja na wananchi ili kudhibiti matukio ya kihalifu.
Ametoa wito kwa wananchi kuendelea kutoa taarifa zitakazosaidia kuwafichua wahalifu kabla hawajatekeleza uhalifu.




