Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) inatarajiwa kutoa huduma za upimaji wa afya ya moyo kwa wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wakati wa Tamasha la Magari la IST litakalofanyika Februari 14, mwaka huu, katika eneo la Coco Beach.
Akizungumza kuhusu tukio hilo, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amesema huduma hiyo inalenga kuwapa wananchi fursa ya kupima afya zao za moyo bila malipo, sambamba na kushiriki katika tamasha hilo linalotarajiwa kuvutia maelfu ya wakazi wa jiji.

Chalamila ameeleza kuwa tamasha hilo litapambwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali pamoja na mashindano ya magari ya IST, ambapo washiriki watapata fursa ya kujishindia zawadi zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 100, ikiwemo magari mapya.
Kwa upande wake, Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Nurdin Bilali Juma maarufu kama Sheta, amesema tamasha hilo ni jukwaa muhimu la kuhamasisha masuala ya afya, burudani na kuimarisha mshikamano miongoni mwa wakazi wa jiji.






