šTanzania Yarudi Kwenye Jukwaa Kubwa Zaidi la Sanaa Duniani na Kuvuta Hisia za Watazamaji wa Kimataifa.
Wasanii wanne wa Tanzania ambao ni Turakella Editha Gyindo, Amani Abeid, Lazaro Samuel na Valerie Asiimwe Amani, wameipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika Maonesho ya 61 ya Kimataifa ya Sanaa ya La Biennale di Venezia, moja ya matukio makubwa na yenye heshima zaidi katika ulimwengu wa sanaa na utamaduni.
Wakiiwakilisha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia banda la taifa lenye maonesho yaliyopewa jina la āMinor Frequencies: The Inner Life of a Nation,ā yaliyodhaminiwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa ushirikiano na Rangi Gallery pamoja na Gervasuti Foundation, wasanii hao hawakufika Venice kama wageni wanaojaribu kujitambulisha. Walifika kama sauti ya uthibitisho kwamba sanaa ya Tanzania ina nafasi yake katika majukwaa makubwa duniani.
Uzinduzi wa maonesho hayo ulihudhuriwa na Balozi wa Tanzania nchini Italia, Balozi Mbarouk Nassor, katika tukio lililoashiria fahari ya taifa na hatua nyingine muhimu kwa Tanzania ambayo inashiriki katika jumba hilo la maonesho la Venice Biennale kwa mara ya pili pekee katika historia yake. Ujumbe wa Tanzania uliongozwa na Kamishna Leah Elias Kihimbi, Naibu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Sanaa kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, akishirikiana na waratibu wa maonesho hayo Lorna Benedict Mashiba pamoja na mratibu kutoka Italia, Martina Cavallarin. Ushirikiano wao ulihakikisha maonesho hayo yanakuwa na ubora wa kimataifa huku yakiwa yamejikita katika simulizi na mazingira ya Tanzania.








Maonesho hayo yalijengwa juu ya wazo la kwamba kile kinachoonekana kuwa kidogo au cha kawaida mara nyingi hubeba maana kubwa zaidi. Katika maelezo yao ya kimtazamo, Mashiba na Cavallarin walieleza kuwa, ākile kinachoitwa kidogo ni cha karibu, cha thamani na hubeba kumbukumbu, pumzi na nguvu ya kustahimili.ā
Maonesho yaligawanywa katika maeneo manne ya tafakuri yaliyounganishwa kwa pamoja: Mwili (The Body), Ishara (The Gesture), Kumbukumbu (The Archive) na Akili (The Mind), ambapo kila msanii aliwakilisha moja ya maeneo hayo.
Turakella Editha Gyindo aliwakilisha dhana ya Mwili ( The body) kupitia kazi yake āTestimonials from the Bodyā. Kazi hiyo ilitumia lufa zilizolimwa na kukatwa kwa mikono na wanawake wa Morogoro, kisha kupakwa rangi za asili zinazotokana na udongo. Matokeo yake yalikuwa tabaka za rangi zinazokumbusha ngozi, ardhi na historia zilizokusanywa kwa muda mrefu. Kazi hiyo inachunguza namna matendo ya kujisafisha yanavyoweza kuwa sehemu ya kumbukumbu, utambulisho na upinzani dhidi ya kufutwa kwa maarifa ya asili.
Kwa upande wake, Valerie Asiimwe Amani aliwakilisha dhana ya Kumbukumbu (The archives) kupitia kazi shirikishi inayokusanya ndoto zilizopotea, kusahaulika au kuachiwa njiani. Wageni wa maonesho wanaalikwa kuandika ndoto au matarajio ambayo waliwahi kuwa nayo lakini baadaye wakayaacha kutokana na changamoto za maisha. Kumbukumbu hizo hukusanywa na kuwa sehemu ya simulizi ya pamoja kuhusu ndoto ambazo hazikuwahi kutimia. Kazi hiyo pia inaambatana na mfumo wa sauti ulioundwa na Jason Langahm ambao huibadilisha taarifa hiyo kuwa sauti zinazoendelea kusikika. Chanzo cha kazi hiyo ni kumbukumbu binafsi ya msanii alipomuuliza baba yake ndoto aliyokuwa nayo utotoni, na kugundua kwamba mazingira ya kupambana na maisha yalikuwa yamefanya ndoto hizo kusahaulika. Kutoka katika simulizi hilo binafsi, kazi hiyo inapanua mjadala kuhusu namna mazingira yanavyoathiri uwezo wa watu kuota na kutimiza ndoto zao.
Lazaro Samuel aliwakilisha dhana ya Ishara (Gestures) kupitia michoro yenye mchanganyiko wa matone, mipasuko na mipigo ya rangi inayofuata hisia na mdundo wa ndani. Safari yake ya maisha, ikiwemo nyakati alizowahi kuishi mitaani jijini Dar es Salaam, ndiyo iliyoipa kazi yake nguvu na uhalisia wa kipekee. Kwa Lazaro, sanaa si taaluma pekee bali ni njia ya kuendelea kuishi. Kila alama ya rangi katika kazi zake hubeba simulizi ya harakati, uvumilivu na matumaini.








Naye Amani Abeid aliwakilisha dhana ya Akili (The Mind) kupitia michoro inayochota msukumo kutoka katika utamaduni wa Kimaasai huku ikiangazia namna jamii za kisasa zinavyoendelea kuathiriwa na tamaduni za dunia. Uwepo wa viatu vya kisigino kirefu katika kazi zake, kama alama ya mvuto wa Magharibi, unawekwa sambamba na alama za utamaduni wa asili ili kuonesha mvutano unaoendelea kati ya urithi wa kitamaduni na mabadiliko ya kisasa. Kupitia kazi hizo, mtazamaji anaalikwa kutafakari namna utambulisho unavyojengwa na kubadilika kati ya kumbukumbu, ushawishi wa nje na hali halisi ya maisha.
Banda la Tanzania lilidhaminiwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa ushirikiano na Rangi Gallery pamoja na Gervasuti Foundation. Rangi Gallery, taasisi ya sanaa ya Tanzania inayozidi kujijengea sifa kimataifa katika kukuza sanaa ya kisasa ya Afrika, imekuwa mhimili muhimu katika kufanikisha maonesho hayo. Ushiriki huu unafuatia mafanikio ya maonesho ya sanaa ya Tanzania yaliyofanyika nchini Korea Kusini na unaonesha kwa wazi kuwa sanaa ya Tanzania inaendelea kupata kutambuliwa kwa kasi katika majukwaa ya kimataifa.
Ushiriki wa Tanzania katika Biennale ya 61 ya Venice ni sehemu ya simulizi kubwa zaidi ya ukuaji wa sekta ya sanaa nchini. Unaonesha kuwa utambulisho wa kisanii wa Tanzania ni mpana, wa kipekee na unaobeba hadithi zenye nguvu zinazovuka mipaka ya nchi.
Maonesho hayo yanaendelea kufanyika katika Gervasuti Foundation at Supernova, Venice, kuanzia tarehe 9 Mei hadi 22 Novemba 2026.








