Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) hivi karibuni imepokea msaada wa darubini ya kisasa ya upasuaji (surgical microscope) kutoka Interplast Germany itakayosaidia katika kufanya upasuaji mgumu unaohusisha mishipa ya damu, taratibu za urekebishaji wa uso na ngozi, pamoja na mfumo wa tezi za kinga.

Kwa mujibu wa Kiongozi wa Mipango kutoka Interplast Prof. Juergen Dolderer, ameeleza kuwa msaada huo umetolewa kama sehemu ya mpango wa kuimarisha huduma na mafunzo ya upasuaji rekebishi nchini Tanzania.
Darubini hiyo, yenye thamani ya shilingi milioni 177 za Kitanzania (sawa na Euro 59,000), inatarajiwa kuboresha kwa kiasi kikubwa huduma za upasuaji wa kibingwa hospitalini hapo.
Akipokea msaada huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa MNH, Daktari bingwa wa upasuaji rekebishi na Mkuu wa Idara ya Upasuaji, Dkt. Ibrahim Mkoma, amesema kuwa msaada huo utachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha ubora wa huduma pamoja na kuongeza uwezo wa kufundisha wataalamu wa fani hizo hapa nchini.




