Sunday, March 8, 2026
spot_img
HomeHabariTaasisi 21 zapatiwa msaada wa zaidi ya Sh. milioni 875 kujikwamua kiuchumi

Taasisi 21 zapatiwa msaada wa zaidi ya Sh. milioni 875 kujikwamua kiuchumi

Dar es Salaam

Taasisi zisizo za kiserikali (NGOs) 21 zimepatiwa msaada wa zaidi ya shilingi milioni 875 kwa ajili ya kujiendeleza kiuchumi na kuisaidia jamii katika jitihada za kufanikisha maendeleo endelevu.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam wakati wa kukabidhi hundi kwa taasisi hizo, Mratibu wa Taasisi ya Nice Tanzania, Seleman Abdullah, alisema msaada huo ni sehemu ya mwendelezo wa programu ya kuwawezesha wadau wa kiraia ili waweze kubadilisha changamoto zinazowakabili kuwa fursa za maendeleo.

Abdullah alifafanua kuwa taasisi yake imekuwa ikiwajengea uwezo wadau hao kwa kuwafundisha namna ya kutambua changamoto zilizopo katika jamii zao, kisha kuzigeuza kuwa miradi yenye manufaa inayowaingizia kipato. Aidha, alibainisha kuwa mapato yatakayotokana na miradi hiyo yatawezesha taasisi husika kuendelea kuisaidia jamii.

“Tuliwafundisha wakaeleza changamoto zilizopo katika jamii yao, wakazitengeneza fursa na sasa zimekuwa miradi ya kujipatia kipato. Kupitia faida watakazopata kutokana na fedha tulizowapa, ambazo tumepatiwa kutoka kwa wafadhili wetu Nama Foundation na Nama Women Advancement, watasaidia jamii zao,” alisema Abdullah.

Aliongeza kuwa wastani wa kila taasisi umepatiwa takribani shilingi milioni 40, huku baadhi zikipewa hadi shilingi milioni 100. Alifafanua kuwa fedha hizo zimetolewa kama mkopo usio na riba, ambapo marejesho yake yataelekezwa kwenye taasisi nyingine zitakazofuata.

“Mchakato huu ulianza Januari na sasa tumewapatia fedha kwa taasisi za Bara na Zanzibar. Tutashirikiana nao kuanzisha miradi waliyoibua ili iweze kuwatengenezea kipato na kugharimia mahitaji yao, huku lengo kuu likiwa ni kuisaidia jamii,” aliongeza.

Abdullah alieleza kuwa taasisi zilizopatiwa msaada huo zinajihusisha na programu mbalimbali ikiwemo uwezeshaji wa wanawake, maendeleo ya kiuchumi, uhifadhi wa mazingira, elimu, afya, pamoja na shughuli za dini na kijamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Nice Foundation, Saleh Bazead, alisisitiza kuwa taasisi zisizo za kiserikali zina mchango mkubwa katika maendeleo ya jamii. Hivyo, ni muhimu kuziwezesha kifedha na kiufundi ili ziweze kutekeleza miradi mbalimbali yenye tija kwa wananchi.

RELATED ARTICLES

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

- Advertisment -
NMB Tanzania

Most Popular

Recent Comments