Baraza kuu la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) limekutana kujadili na kuweka mwelekeo wa vipaumbele vya Mamlaka kuelekea mwaka wa fedha 2026/2027, likilenga kuimarisha utoaji wa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi.
Akizungumza katik kikao kazi hicho, Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Mwajuma Waziri, amesema Baraza la wafanyakazi ni jukwaa muhimu la mawasiliano linalowaunganisha Menejimenti na watumishi katika kupanga mikakati ya kuboresha huduma kwa wananchi.
“Niwashukuru kwa kunialika kuwa mgeni rasmi katika tukio hili. Ni matumaini yangu kuwa majadiliano yenu yatajikita katika kukabiliana na changamoto ya upotevu wa maji ili kuimarisha huduma na kuokoa mapato yanayopotea,” amesema Mhandisi Mwajuma.




Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa DAWASA, Mhandisi Romanus Mwangingo, amesema kipaumbele kikuu cha Mamlaka kwa sasa ni kukabiliana na changamoto ya upotevu wa maji, akibainisha kuwa tayari hatua mbalimbali zimeanza kuchukuliwa.
“Tunawekeza katika kupunguza upotevu wa maji kwa kununua mita za malipo ya kabla kwa ajili ya wateja na kubadilisha miundombinu chakavu ambayo imekuwa ikichangia upotevu huo,” amesema Mhandisi Mwangingo.
Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi Mkama Bwire, amewashukuru viongozi wa sekta ya maji kwa kushiriki katika uzinduzi wa kikao hicho, na kuwataka wajumbe wa Baraza la wafanyakazi kushirikiana kikamilifu katika utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa.
“Ni muhimu kila mmoja wetu akawa sehemu ya suluhisho kwa kutoa elimu kwa watumishi wenzake ili kusimama kwa pamoja katika kukabiliana na changamoto ya upotevu wa maji,” amesema Mhandisi Bwire.








