Halmashauri ya Mji wa Handeni imeandaa bonanza kubwa la michezo lenye lengo la kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29 mwaka huu.
Bonanza hilo limefanyika leo katika Uwanja wa Kigoda, Handeni, likihusisha wananchi, watumishi wa umma, viongozi wa dini, viongozi wa kisiasa pamoja na taasisi binafsi.

Akizungumza katika bonanza hilo, Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Salum Nyamwese, amewahimiza wananchi wote waliojiandikisha kuhakikisha wanajitokeza kupiga kura ili kutimiza haki yao ya kikatiba ya kuchagua viongozi wanaowataka.
“Nawasihi wananchi wote wa Handeni kujitokeza mapema siku ya uchaguzi. Vituo vitafunguliwa saa 1:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni. Serikali imeimarisha ulinzi na usalama, hivyo kila mmoja atapiga kura kwa amani na utulivu kama tulivyoshiriki bonanza letu leo. Hakuna mwananchi atakayebugudhi,” amesema Nyamwese.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Handeni, Maryam Ukwaju, amesema lengo la bonanza hilo ni kuongeza mwamko wa wananchi kushiriki kikamilifu katika uchaguzi wa Oktoba 29, 2025, ili kutimiza haki yao ya kikatiba.






