Wataalamu wa biashara ya mafuta duniani wameonya kuwa mabadiliko ya bei za rejareja za mafuta huenda yakachelewa kuonekana kwa watumiaji wa kawaida, licha ya bei ya mafuta ghafi kuanza kushuka katika soko la dunia.
Wachambuzi hao wamesema nchi nyingi zinazoagiza mafuta kupitia masoko ya kimataifa, hususan zinazotegemea usafirishaji kupitia Mlango wa Hormuz, zinaweza kuchukua kati ya wiki nane hadi kumi kabla ya kuona mabadiliko makubwa ya bei kwenye vituo vya mafuta.
Kwa mujibu wa taarifa za masoko, bei ya mafuta ghafi aina ya Brent imeshuka hadi dola 73.49 kwa pipa, ikiwa ni kiwango cha chini zaidi tangu kabla ya kuongezeka kwa taharuki za kisiasa zilizohusisha Iran, Marekani na Israel, baada ya awali kupanda zaidi ya dola 100 kwa pipa.
Wachambuzi wanaeleza kuwa kushuka huko kumechangiwa na kupungua kwa hofu ya kuvurugika kwa usambazaji wa mafuta, kuendelea kwa mazungumzo ya kidiplomasia pamoja na kurejea kwa usafirishaji wa mafuta kupitia Mlango wa Hormuz, ambao hupitisha takribani asilimia 20 ya mafuta ya dunia.

Hata hivyo, Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) limesema kuwa ingawa kushuka kwa bei kumeanza kuonekana katika soko la dunia, athari kwa watumiaji wa mwisho itachukua muda kutokana na mnyororo mrefu wa biashara ya mafuta unaojumuisha usafirishaji, usafishaji, uhifadhi na usambazaji.
Wataalamu wa sekta hiyo wanasema mafuta yanayouzwa leo mara nyingi huwa yameagizwa wakati bei ilikuwa juu, hivyo kushuka kwa bei kwenye vituo vya mafuta huanza kuonekana baada ya shehena mpya zilizonunuliwa kwa bei ya chini kuingia sokoni.
Mchambuzi wa masoko ya nishati wa Rystad Energy, Janiv Shah, amesema kuimarika kwa usafirishaji kupitia Ghuba ya Uajemi kumeongeza upatikanaji wa mafuta sokoni, huku UBS ikisisitiza kuwa hali ya usalama na gharama za bima bado ni vikwazo vinavyoweza kuchelewesha kurejea kwa bei za kawaida.
Kwa sasa, wachambuzi wanasema mwenendo wa soko unaashiria utulivu wa taratibu, lakini wakisisitiza kuwa mabadiliko yoyote ya kisiasa au kiusalama katika Mashariki ya Kati yanaweza kubadili tena mwenendo wa bei za mafuta duniani.






