Mbunge wa Tunduru Kaskazini, Ado Shaibu Ado, ameitaka Serikali kuzingatia maslahi ya mahakimu, majaji na majaji wastaafu ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa weledi na ufanisi.
Amesema masuala ya maslahi ya watumishi wa mhimili wa mahakama hayapati kipaumbele cha kutosha, akitaja umuhimu wa kufanya mapitio ya mishahara, kuboresha makazi, posho za makazi pamoja na upandaji wa madaraja kwa wakati.
Aidha, ameishauri Serikali kuboresha mfumo wa usimamizi wa mahakama kwa kurekebisha sheria ili kuondoa utaratibu wa kamati za maadili ya mahakimu kuwa chini ya Wakuu wa Wilaya na Mikoa ambao ni wanasiasa.
Ado amependekeza kuanzishwa kwa mfumo wa mahakama kujisimamia yenyewe (self-regulation), akieleza kuwa hatua hiyo itaongeza uhuru wa mhimili wa mahakama na kuimarisha haki na utawala bora nchini.




