CRDB Bank Plc imetwaa tuzo ya Benki Bora inayowahudumia Wateja wa Hadhi ya Juu Tanzania 2026, iliyotolewa na Euromoney, hatua inayoonesha ubora wa huduma zake katika sekta ya fedha.
Tuzo hiyo ilikabidhiwa nchini Uingereza, ambapo Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, alisema mafanikio hayo yanatokana na ubunifu na umakini katika kuwahudumia wateja wa makundi mbalimbali.
Amesema benki hiyo itaendelea kuboresha huduma na bidhaa zake ili kukidhi mahitaji ya wateja, hususan wa hadhi ya juu, kwa kuongeza vituo maalum vya huduma nchini kote.


Kwa sasa, CRDB ina vituo zaidi ya 50 vya kuwahudumia wateja wa hadhi ya juu ndani ya mtandao wa matawi zaidi ya 260, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kusogeza huduma karibu na wananchi.
Dkt. Nsekela amesema ushindi huo ni zaidi ya mafanikio ya benki, bali ni ishara kuwa taasisi za kifedha za Tanzania zina uwezo wa kushindana kimataifa.












