Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Tafiti na Uchumi Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dk. Suleiman Misango, ameshangazwa na jinsi Mfumo wa PSSSF Portal, ulivyoweza kutoa taarifa za wanachama wa PSSSF kwa haraka tangu alipoanza ajira hadi hivi sasa.
Ameyasema hayo, Agosti 4, 2026 wakati akitoa maoni yake jinsi anavyohudumiwa na Mfuko, mbele ya Kaimu Mkurugenzi wa Uendeshaji Mfuko wa PSSSF,Hajj Moshi, aliyekuwa katika ziara ya Banda kwa Banda inayofanywa na PSSSF kuwatembelea wanachama wake kwenye mabanda ya Maonesho ili kuwahudumia na kupokea maoni yao, katika Viwanja vya Dk. John Malecela, Nzuguni jijini Dodoma.
” Mimi ni Mwanachama wa PSSSF wa muda mrefu, lakini nimeshangazwa sana, nilipotaja tu jina langu, taarifa zangu zote zikaonekana kwenye mfumo kwa spidi ya ajabu,” alisema baada ya kuhudumiwa kupitia mfumo ya PSSSF Portal.

Alipongeza hatua kubwa iliyopigwa na PSSSF ambapo Mfumo huo umewezesha kupatikana kwa taarifa bila ya usumbufu wowote.
”Ingekuwa zamani huyu dada angeanza kuhangaika huku na kule kutafuta mafaili, lakini hapa ame press button na kila kitu kimetokea. Ninaweza kusema mfumo huu ume decentralise huduma, na sio lazima huduma zifuatwe mahala pamoja bali zinapatikana popote kupitia PSSSF Portal, nimeona taarifa zangu tangu nimeanza ajira hadi hivi sasa, hongereni sana.” Alipongeza Dk. Misango ambaye ni Mchumi aliyebobea.


Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Uendeshaji PSSSF, Hajj Moshi, amesema, moja ya ajenda kubwa ya Mfuko ni kuendelea kuwahamasisha wanachama kutumia teknolojia hiyo ya kisasa ya PSSSF Portal kujihudumia popote na wakati wowote, na huduma hii imeleta ufanisi mkubwa.
” Sasa hivi tunakwenda na kampeni ya “Tunalipa Jana”, ambayo inawezeshwa na utunzaji mzuri wa kumbukumbu, matumizi ya PSSSF Kidijitali na uwezo wa kifedha ambao Mfuko unao.” alisema.


Ndio maana tunapokuwa na Maonesho kama haya, tunatumia fursa hiyo kuwaelimisha na kuwaunganisha wanachama na Mfumo wa Huduma za Kidijitali.” alisema.
Alisema, PSSSF Portal imeweza kukidhi mahitaji ya sasa ya wanachama, hususan vijana wa kizazi cha sasa ambao wako kwenye ulimwengu wa teknolojia.
Mabanda aliyotembelea ni pamoja na lile la Taasisi ya Vyuo Vikuu na Ofisi ya Rais lakini pia Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI).





