Bahi, Dodoma: Serikali imeipongeza NMB Bank Plc kwa kujenga shule ya sekondari ya bweni kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu wilayani Bahi, mradi wa Sh5 bilioni uliokamilika kwa asilimia 100.
Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Elimu, Atupele Mwambene, amesema shule hiyo imejengwa kwa kiwango cha juu na ina mabweni, vitanda, madawati pamoja na uwezo wa kuhudumia wanafunzi 160. Inatarajiwa kuanza kupokea wanafunzi Januari 2027 baada ya usajili.
Mkurugenzi wa Uhusiano na Wawekezaji, Uendelevu na Mawasiliano wa NMB, Innocent Yonazi, amesema mradi huo unalenga kupanua fursa za elimu kwa watoto wenye mahitaji maalumu. NMB imetoa zaidi ya Sh24 bilioni kwa miradi ya kijamii katika miaka mitano.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Bahi, Albina Mtumbuka, amesema halmashauri iko tayari kuipokea na kuitunza shule hiyo, huku akiwataka wazazi kutowaficha watoto wenye mahitaji maalumu.











