HomeHabariBunge Laitaka Serikali Kuongeza Wataalamu OSHA

Bunge Laitaka Serikali Kuongeza Wataalamu OSHA

DODOMA. Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii imeishauri Serikali kuiongezea wataalam Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) ili Taasisi hiyo iweze kuimarisha afya, usalama na ustawi wa wafanyakazi nchini.

Ushauri huo umetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Hawa Chakoma, Bungeni Jijini Dodoma (Agosti 12, 2026), alipokuwa akifungua kikao cha Kamati kilicholenga kupitia taarifa ya utekelezaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi, Sura Namba 297, Toleo ya 2023 ikiangazia mwenendo wa usajili wa maeneo ya kazi pamoja na utoaji wa elimu ya usalama na afya mahali pa kazi kwa umma kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Taarifa hiyo iliwasilishwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu ambaye aliambatana na wataalam katika Ofisi yake akiwemo Katibu Mkuu, Bi. Mary Maganga na Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda.

Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa na Waziri Sangu mbele ya Kamati hiyo, kwa mwaka fedha 2025/2026, OSHA imesajili maeneo ya kazi 16,813 na kutoa mafunzo ya usalama na afya kwa wadau wapatao 45,089 idadi ambayo ni zaidi ya lengo ya kuwafikia wadau 40,000.

Akitoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja za wajumbe wa Kamati, Mtendaji Mkuu wa OSHA amesema maeneo ya kazi yanayosajiliwa na OSHA yanapaswa kukidhi vigezo vilivyowekwa kikiwemo kigezo cha uwepo wa pande mbili zinazotegemeana ambazo ni mwajiri na mwajiriwa.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Hawa Chakoma, alipokuwa akifanya majumuisho ya michango ya Wajumbe wa Kamati, ameishauri Serikali kuiongezea Taasisi ya OSHA watumishi ili kuiwezesha kutekelezaja majukumu yake ipasavyo kutokana na watumishi 376 waliopo kutokidhi mahitaji ya watendaji wa shughuli za msingi za Taasisi hiyo.

“Tunatambua kazi kubwa inayofanywa na OSHA katika kutoa miongozo inayolenga kuimarisha mifumo ya usalama na afya katika maeneo ya kazi nchini lakini tunaona idadi ya watumishi waliopo hususan wakaguzi wa usalama na afya haitoshelezi kuhudumia maeneo yote ya kazi nchini,” ameeleza Mhe. Chakoma.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, amesema serikali imejipanga kuendelea kuhamasisha uzingatiaji wa taratibu zote muhimu za usalama na afya kwa waajiri na wafanyakazi katika sekta ya umma na binafsi.

“Kwenye ukaguzi wa usalama na afya mahali pa kazi hakuna upendeleo kati ya sekta ya umma na sekta binafsi kwasababu usalama na afya unawahusu wafanyakazi wote. Hivyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mwenyekiti na Kamati yako kwamba tutaendelea kusimamia utekelezaji wa sheria katika maeneo yote bila kujali endapo yanamilikiwa na serikali au watu binafsi,” amefafanua Waziri Sangu.

Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Bi. Mary Maganga, amewataka watumishi wapya wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kuzingatia maelekezo ya msingi waliyopatiwa katika mafunzo ya awali (induction training) yaliyotolewa kwa lengo la kuwaandaa kutekeleza majukumu yao ipasavyo katika utumishi wa umma.

Katibu Mkuu ametoa wito huo wakati akifungua mafunzo ya wiki moja kwa watumishi wapya 55 pamoja na tisa waliohamia kutoka Taasisi nyingine.

Bi. Maganga amesema mafunzo hayo ni muhimu kwa watumishi hao kwa kuwa yanawajengea uwezo wa kufanya kazi vizuri na kuwasaidia kuelewa mazingira ya utumishi wa umma.

Aidha, amewaasa kuepuka tabia zisizokubalika katika utumishi wa umma ikiwemo kutumia lugha zisizofaa wanapotoa mchango wao wa mawazo ambapo amesihi kutumia lugha ya staha na kutoa Mawazo Chanya yatakayoisaidia Taasisi kupiga hatua katika utendaji wake.

Kamati ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii imekuwa ikiishauri serikali juu ya maboresho mbalimbali yanahitajika katika Taasisi ya OSHA likiwemo suala ya kuongeza idadi ya watumishi ambapo ajira hizo mpya ni utekelezaji wa maagizo hayo ya Kamati ambapo zaidi ya watumishi 116 wameajiriwa ndani ya miaka miwili huku mchakato wa kuajiri watumishi zaidi ukiendelea. Aidha kama sehemu ya mpango wa serikali wa kuijengea uwezo Taasisi ya OSHA, serikali imefanikisha upatikanaji wa vifaa vya kisasa vya ukaguzi vyenye thamani ya bilioni 2.2 ndani ya kipindi cha miaka mawili.

RELATED ARTICLES

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

- Advertisment -
NMB Tanzania

Most Popular

Recent Comments