Kemikali za sumu zinazojificha kwenye vifaa vya plastiki vinavyotumika kila siku kuanzia midoli ya watoto hadi vyombo vinavyogusana na chakula zinatajwa kuwa tishio kubwa kwa afya ya binadamu na mazingira katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Wataalamu wa mazingira wanasema ingawa plastiki nyingi hufikiriwa kuwa salama na zenye uwezo wa kurejelewa, baadhi ya bidhaa hizo zina kemikali hatarishi ambazo huweza kuchafua bidhaa nyingine zinazotengenezwa kutokana na plastiki iliyorejelewa, hali inayoongeza hatari ya kuathiri afya ya watumiaji, hasa watoto wanaocheza na midoli au familia zinazotumia vyombo vya plastiki jikoni.
Ni kutokana na wasiwasi huu ndipo wadau wa mazingira kutoka Kenya na Tanzania, wakishirikiana na mashirika ya kimataifa, wamezindua mradi mpya wenye lengo la kukabiliana na tatizo hilo kwa kujenga uchumi rejeshi wa plastiki usio na sumu.
Mradi huo, “Advancing a Non-Toxic Circular Economy in East Africa,” umeandaliwa na Centre for Environment Justice and Development (CEJAD) ya Kenya kwa kushirikiana na AGENDA for Environment and Responsible Development ya Tanzania, pamoja na washirika wengine akiwemo International Pollutants Elimination Network (IPEN), Arnika kutoka Jamhuri ya Czech, na Environmental Coalition on Standards (ECOS). Unafadhiliwa na Basel Convention Plastic Waste Partnership na utatekelezwa kwa miezi 18.
Mkurugenzi wa CEJAD, Griffins Ochieng, alisema uwepo wa kemikali hatarishi katika baadhi ya bidhaa za plastiki unaweza kuzifanya zisifae kwa mfumo salama wa uchumi rejeshi, licha ya plastiki kutambulika kama nyenzo yenye thamani kiuchumi.
Mradi utafanya kazi katika maeneo matatu makuu: kutathmini mifumo ya usimamizi wa taka za plastiki huku ukifanya ufuatiliaji wa kemikali hatarishi katika bidhaa zilizochaguliwa; kujenga uwezo wa wadau katika uandaaji wa viwango na hatua za udhibiti, ikiwemo Wajibu wa Mtengenezaji kwa Bidhaa Anazozalisha (EPR); na kusambaza ushahidi na mapendekezo katika ngazi za kitaifa, kikanda na kimataifa.
Clara Benjamin, Afisa Programu wa AGENDA na Mratibu wa mradi Tanzania, alisema mradi pia utasaidia kuandaa kiwango cha kikanda kupitia Kamati ya Viwango ya Afrika Mashariki, kitakachosaidia nchi wanachama wa EAC kutofautisha plastiki salama na zile zenye kemikali hatarishi.
Wadau wanatarajia matokeo ya mradi kusaidia kuimarisha udhibiti wa kemikali hatarishi tangu chanzo na kujenga mfumo wa plastiki unaolinda afya ya jamii na mazingira ya ukanda huu.




