Mbunge wa Segerea (CHAUMA), Agnesta Lambert, amesema atawasilisha bungeni changamoto ya upungufu wa mabweni inayowakabili wanafunzi viziwi katika Shule ya Msingi Viziwi Buguruni jijini Dar es Salaam.
Ameeleza hayo leo, Machi 17 jijini Dar es Salaam wakati akikabidhi msaada wa vyakula na mahitaji muhimu kwa wanafunzi hao, ikiwa ni sehemu ya kuwawezesha kusherehekea kwa furaha na heshima Sikukuu za Idd el-Fitr na Pasaka.
Amebainisha kuwa moja ya changamoto kubwa inayoikabili shule hiyo ni upungufu wa mabweni kwa wanafunzi, hivyo katika bunge lijalo la bajeti atawasilisha changamoto hiyo ili iweze kutatuliwa.




Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele katika sekta ya elimu, hivyo ana matumaini changamoto hizo zitapatiwa ufumbuzi.
Agnesta amesema anajisikia kuwajibika kusimamia masuala ya kijamii hususani kwa watoto wenye mahitaji maalum, akisisitiza kuwa uwekezaji katika elimu na ustawi wao ni msingi wa kujenga jamii jumuishi yenye usawa wa fursa.


Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu Msaidizi wa shule hiyo, Richard Kweka, amesema uhaba wa mabweni unawaweka wanafunzi katika hatari mbalimbali ikiwemo ajali, kutokana na mazingira yasiyo rafiki kwa hali yao.
Baadhi ya wanafunzi katika shule hiyo akiwamo Salehe Abdallah na Faine Robert wametoa wito kwa jamii na wadau mbalimbali kuendelea kuwasaidia watoto wenye mahitaji maalum, wakisisitiza umuhimu wa mshikamano wa kijamii katika kujenga mustakabali bora kwa wote.





