Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka, ameziomba taasisi za kifedha kusaidia upatikanaji wa mashine za kusafisha damu — dialysis — katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe ili kupunguza gharama kwa wagonjwa wanaofuata huduma hiyo Mbeya.
Mtaka ametoa ombi hilo Aprili 28, 2026, wakati akipokea vifaa vya shule na hospitali vilivyotolewa na Benki ya NMB. Alisema taasisi za ndani zina uwezo wa kugusa maisha ya wananchi moja kwa moja kupitia uwekezaji kwenye afya na elimu.


Meneja wa NMB Kanda ya Nyanda za Juu, Wagofya Mfalamagoha, amesema benki hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali kutatua changamoto za kijamii. NMB imetoa Sh milioni 80 kusaidia maandalizi ya Mei Mosi kitaifa Njombe na Sh milioni 120 kwa vifaa vya shule na hospitali.
Mganga Mkuu wa Mkoa, Dk. Juma Mfanga, amesema ukosefu wa mashine za dialysis ni changamoto kubwa kwa wagonjwa wa figo kutoka Njombe na mikoa jirani. Ofisa Elimu Mkoa, Nelasi Mulungu, aliishukuru NMB kwa madawati 400, pamoja na viti na meza kwa shule za sekondari.





