Kiungo wa Newcastle United, Bruno Guimarães, ameonyesha dhamira ya kubaki klabuni hapo kwa muda mrefu zaidi huku akiwa tayari kuanza mazungumzo ya kuongeza mkataba.
Guimarães, ambaye pia ni nahodha wa timu hiyo, hana mpango wa kudai mshahara mkubwa katika mkataba mpya, jambo linaloashiria utayari wake wa kuendelea kuitumikia Newcastle.
Hivi karibuni kumekuwa na tetesi za kuwindwa na Manchester United, ambayo inatafuta mbadala wa Casemiro anayetajwa huenda akaondoka mwishoni mwa msimu.
Hata hivyo, msimamo wa Guimarães unaweza kuwa pigo kwa United, ambayo bado inatafuta mchezaji sahihi wa kuziba pengo hilo licha ya kuwa na orodha ya wachezaji inaowahitaji.
Mkataba wa nyota huyo unatarajiwa kumalizika mwaka 2028, huku Newcastle ikitajwa kuhitaji takribani pauni milioni 100 iwapo itamuuza. Tangu kuanza kwa msimu huu, Guimarães amecheza mechi 35 katika mashindano yote.




